MWANDISHI WETU
Dar es Salaam
SIKUKUU ya Krismasi si ndiyo leo?
Jibu ni ‘ndiyooooo!’, sasa habari kamili ni kuwa wakazi wa Dar es Salaam
na maeneo ya jirani, wote wanatarajiwa kukutana kwenye Ukumbi wa Dar
Live, Mbagala-Zakhem ambapo Simba wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond
Platnumz’ atakuwa akifanya makamuzi.
Diamond, staa ambaye anasadikika
kupata umaarufu mkubwa nje ya mipaka ya nchi zaidi ya wasanii wengi wa
Bongo Fleva katika historia ya muziki huo, atakuwa akitambulisha kwa
mara ya kwanza wimbo wake wa Utanipenda?
Meneja wa Dar Live, Juma
Mbizo amefunguka kuwa burudani itaanza rasmi asubuhi maalum kwa watoto
ambapo kutakuwa na michezo mingi ikiwemo kuteleza, kubembea, kupanda
ndege maalum, kuogelea kwenye bwawa kubwa la kisasa na mingine mingi.
“Watoto
wote wanaruhusiwa kuja kwa kiingilio kidogo cha shilingi 2,000 tu na
kupata burudani zote hizo hadi saa kumi na mbili jioni kisha
itafunguliwa rasmi shoo ya wakubwa,” anasema Mbizo.
Diamond:
Nitakamua shoo live
Kuelekea
shoo yake ya leo pale Dar Live, Diamond anasema: “Kwanza nitatoa zawadi
kwa mashabiki wote watakaotoka bomba siku ya shoo ikiwa ni pamoja na
kupiga nao picha na kuzungumza nao mawili matatu kabla sijapanda
jukwaani.
“Pia nitafanya shoo ya ‘live’, ambapo nitakuwa pamoja na
timu yangu nzima ya Wasafi Classic Baby (WCB). Ngoma zangu zote kali
nitaziimba zikiwemo Mbagala, Mdogomdogo, Nasema Nawe, Nana, Nitarejea,
Nataka Kulewa, Kesho, Moyo Wangu na huu ambao ni wimbo wa taifa kwa
sasa, Utanipenda?”
Msagasumu, Diamond uso kwa uso
Bingwa wa muziki wa Singeli, Msagasumu naye atakuwepo jukwaani kupiga shoo kali.
Unajua
amesemaje jamaa? Ah ah ah ah ana mbwembwe balaa, msikie hapa. “Siku
zote nikiwa Dar Live huwa sikosei, nitapiga ngoma zote kuanzia Shemeji
Unanitega, Huyu Mtoto, Inaniuma Sana na Naipenda Simba, yaani kwa ufupi
nitafunikaaa!”
Wakali Dancers kudansi 100%
Kuthibitisha kuwa
Sikukuu ya Krismasi inakwenda vizuri, mashabiki pia wategemee kuliona
kundi linalobamba Afrika Mashariki upande wa kudansi, Wakali Dancers nao
watakuwa jukwaani kufanya kweli.
Mshindi Ijumaa Sexiest Girl huyu hapa
Wafuatiliaji
wa shindano la mwanamke mwenye mvuto (Ijumaa Sexiest Girl 2015)
linaloendeshwa na Gazeti la Ijumaa kwa mara nyingine watapata fursa ya
kuwashuhudia live washiriki wote walioshiriki shindano hili sambamba na
kutangazwa mshindi.
Shindano hili ambalo limedhaminiwa na Hamadombe
Distributor limebakiwa na washiriki watatu walioingia fainali ambao ni
Asha Salum ‘Kidoa’, Elizabeth Michael ‘Lulu’ na Vanessa Mdee ‘Vee
Money’, leo usiku mshindi atajulikana.
Miongoni mwa zawadi
atakazoibuka nazo mshindi wa shindano hili ni fedha taslim, tuzo, cheti,
ofa ya bure ya kufanya shopping ya nguo na kutengenezwa nywele kwa
kipindi cha miezi sita.
Unaingiaje Dar Live? Soma hapa
Burudani yote hiyo itakuwa ni kwa kiingilio cha shilingi 15,000 (kawaida) huku V.I.P ikiwa ni shilingi 30,000 tu.
Mbali
na kiwango hicho, wadhamini wakuu wa shoo hii ambao ni Kampuni ya
Mawasiliano ya Simu za Mkononi Airtel, kupitia huduma yao ya kijanja
kimawasiliano ya Airtel Money Tap Tap watatoa punguzo la kiingilio kwa
tiketi 1,000 za awali endapo utakata kwa kutumia huduma hiyo mpya.
Unachopaswa
ni kuwa na kadi yako ya Airtel Money Tap Tap ambayo inapatikana kwa
mawakala wote wa Airtel waliopo Temeke na Ilala na ukifika nayo Dar Live
utapata punguzo la Sh 5,000 yaani tiketi ya Sh 15,000 utapata kwa Sh
10,000 na ya Sh 30,000 itakuwa Sh 25,000.
No comments:
Post a Comment
paulmkale